.

Jumatatu, 6 Oktoba 2014

UTAPELI MZITO: WABONGO WALIZWA 'MIKOPO YA OBAMA, JK'



Rais Jakaya Mrisho Kikwete akiwa Rais Barack Obama wa Marekani .
Stori: Harun Sanchawa na Hamida Hassan
Utapeli mzito umeshamiri Bongo ambapo imebainika kuna taasisi iliyojipachika jina la Tanzania Loan Society inayojieleza kuwa inafadhiliwa na Serikali ya Tanzania kwa ushirikiano wa Serikali ya Marekani huku ikiwarubuni watu kuwa inatoa mikopo bila riba.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dk Jakaya Mrisho Kikwete. Ipo kimtandao zaidi
Taasisi hiyo iliyoanzishwa muda mrefu ikapotea, sasa imeibuka upya na inawaliza wengi ambapo inaendesha shughuli zake kimtandao na wahusika hutumia utundu kuingilia mawasiliano katika akaunti za watu katika facebook na kuweka ushuhuda kuwa wamiliki wamefanikiwa kupata mkopo bila riba tena kwa masharti rahisi.
Mtandao umegundulikaje?
Mmoja wa wasomaji wa gazeti hili aliyefahamika kwa jina la Lulu, hivi karibuni alileta malalamiko yake akieleza jinsi wahusika wa utapeli huo walivyoingilia mawasiliano yake ya Facebook, wakamlisha maneno kuwa aliomba mkopo wa shilingi milioni 3 baada ya kutoa shilingi 95,000 kwa ajili ya uanachama na akapewa fasta.
Kwenye ukurasa wa Facebook wa Lulu, kulikuwa na maelezo ya kupika kuwa, Tanzania Loan Society ni taasisi iliyo chini ya Rais Jakaya Kikwete kwa msaada wa Rais wa Marekani Barack Obama huku watendaji wakuu wakiwa ni Waziri Mkuu, Mhe. Mizengo Pinda na Mbunge wa Chalinze, Mhe.
Ridhiwani Kikwete.
Ikadaiwa eti muweka hazina wa taasisi hiyo ni Zainabu Kikwete huku namba zake za simu zikitajwa kuwa ni 0767 602 518 na 0713 009 819, lengo la mpango huo likiwa ni kuhakikisha Watanzania wanaondokana na umaskini kwa kupewa mikopo kwa masharti nafuu.
Chini ya maelezo hayo kuna linki ya kuingia kwenye mtandao wa taasisi hiyo feki (ambapo ukiufungua unakuta nembo ya serikali ya Tanzania na maelezo yanayomshawishi mtu yeyote kuamini kuwa siyo ishu ya kitapeli.
Kinachomsukuma mtu kuingia mtegoni ni kwamba, kwanza wanahusishwa viongozi wakubwa, pili matapeli hao wanaeleza kuwa makao makuu ya taasisi hiyo ni Posta jijini Dar kwenye jengo la Utumishi, ghorofa ya 5, chumba namba 30 na anayehitaji mkopo kuanzia laki moja hadi milioni 50 anatuma 95,000 kupitia namba za muweka hazina (Zainabu Kikwete feki).
Risasi laingia kazini
Baada ya kupatikana kwa taarifa hizo, Septemba 28, mwaka huu, waandishi walianza uchunguzi kwa kuthibitisha kama namba za Zainabu zimesajiwa kwa jina gani ambapo ilionekana imesajiliwa kwa jina la Zainabu Kikwete.

Kisha mwandishi wetu alimpigia Zainabu, alipopokea na kuulizwa kuhusiana na taasisi hiyo alisema ni kweli ipo na maelezo yote yapo kwenye mtandao wao huku akimsisitiza mwandishi kutuma pesa ili atumiwe mkopo.

Waandishi watinga Jengo la Utumishi
Baada ya kujiridhisha, waandishi wetu walimpigia tena Zainabu na kumtaarifu kuwa wapo njiani kuelekea ofisini kwao, kwa kujiamini alisema hakuna shida na kama ni mkopo upo unawasubiria.
Baada ya waandishi wetu kufika kwenye jengo la Utumishi, walimpigia tena simu Zainabu kumjulisha kuwa wameshafika ambapo alidai wametoka kidogo ofisini (eti wameenda kukusanya madeni sugu) na kwamba wakutane kesho yake.
Waandishi wetu wakiwa nje ya jengo hilo, waliongea na mmoja wa walinzi na kumuuliza juu ya uwepo wa taasisi hiyo ambapo alieleza kuwa, haipo na wengi wamekuwa wakifika hapo baada ya kutapeliwa.
Ili kupata taarifa rasmi, waandishi walifika kwenye ofisi ya mmoja wa maafisa habari wa Ofisi ya Rais, Menejimenti na Utumishi wa Umma, Florence Laurence ambaye alikiri taasisi hiyo ya kitapeli kuhusisha jengo lao na walishatoa tahadhari kwa wananchi.
Msako wafanyika
Licha ya majibu yaliyotolewa na afisa habari huyo, waandishi wetu walifika katika Ofisi ya Polisi, Kanda Maalum ya Dar, Kitengo cha Intelijensi na kutoa taarifa ambapo walichukua taarifa kuhusiana na mtandao huo na kuahidi kudili nao.
Septemba 30, mwaka huu ofisi hiyo ilitoa polisi wawili ambao waliongozana na waandishi wetu mpaka katika jengo la Utumishi na mhusika alipopigiwa simu alidai siku hiyo pia walikuwa bize kukusanya madeni sugu na kwamba waende tena kesho yake.
Kutokana na kuchengachenga kwa wahusika, polisi walishauri waachwe wafanye kazi yao na kwamba kwa mbinu zao za kiintelijensia watawanasa wahusika. Uchunguzi wa gazeti hili umebaini kuwa, mtandao huu umewaliza wengi hivyo ni vyema watu wakawa makini. - See more at: http://winternews1.blogspot.com/2014/10/utapeli-mzito-wabongo-walizwa-mikopo-ya.html#sthash.tS4H3zTr.dpuf

0 comments:

Chapisha Maoni